Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Umoja wa Mataifa walaani shambulizi kwa ubalozi wa Ufaransa nchini Libya

Umoja wa Mataifa walaani shambulizi kwa ubalozi wa Ufaransa nchini Libya

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki-moon, amelaani vikali shambulizi dhidi ya ubalozi wa Ufaransa mjini Tripoli leo April 23, na kutuma risala ya pole kwa familia na wahanga. Katika taarifa ilotolewa na msemaji wake, Bwana Ban amesema mshambulizi dhidi ya balozi za kigeni na wafanyakazi wake hayakubaliki. Taarifa hiyo pia inasema

Katibu Mkuu anaamini kuwa mamlaka za Libya zitafanya kila hatua kuhakikisha kuwa walotekeleza shambulizi hilo wanakabiliwa na mkono wa sheria, na kuweka ulinzi tosha kwa balozi za kigeni. Ametoa wito kwa raia wa Libya waunge mkono juhudi za serikali yao za kuweka taasisi imara za usalama.

Wakati huo huo, wanachama wa Baraza la usalama wamelilaani shambulizi hilo, na vitendo vyote vya ghasia dhidi ya wawakilishi wa kidiplomasia.

Wanachama hao wamesema ugaidi wa aina yoyote ile ni moja wa tishio kubwa zaidi kwa amani na usalama, na kwamba vitendo vyote vya ugaidi ni uhalifu na havikubaliki, bila kujali kinachovichochea, wapi vinapofanyika, au nani kavifanya.