Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Nchi isipolipa deni inaweka rehani vizazi vijavyo: UNCTAD

Nchi isipolipa deni inaweka rehani vizazi vijavyo: UNCTAD

Baraza la kijamii na kiuchumi la Umoja wa Mataifa ECOSOC leo limekuwa na mjadala kuhusu deni la nje ambapo washiriki wameangalia yale waliyojifunza kutokana na nchi kupata mikopo ya kigeni, athari zake na mchakato wa kufanya mikopo ya kigeni kuwa na manufaa zaidi kwa nchi husika na dunia kwa ujumla. Akitoa hotuba katika mkutano huo, Katibu Mkuu wa shirika la biashara na maendeleo la Umoja wa Mataifa, UNCTAD Supachai Panitchpakdi amesema ukopaji wenye  uwajibikaji unaweza kuwa njia nzuri ya kuboresha sera ya uchumi na kwamba urejeshaji wa mkopo unaweza kuchochea vitegauchumi na ukuaji wa uchumi.  Hata hivyo amesema kuna changamoto katika urejeshaji mikopo hususan kutoka nchi zilizoendelea kutokana na ukosefu wa ajira.

 (SAUTI YA SUPACHAI)

 

“Ongezeko la idadi ya watu wasio na ajira kwenye nchi zilizoendelea! Hili ni jambo lingine ambalo linahusiana na suluhisho la kifedha. Kile tunachohitaji katika sekta mahsusi.. tunahitaji kuona uwezeshaji mpya wa kifedha na kistadi na vitegauchumi vipya ili kuweza kushughulikia changamoto mpya za kifedha. Hatuwezi kuzishughulikia changamoto hizo kwa fedha pekee na hilo ni somo ambalo tumejifunza na hatukuwa tumejifunza miaka ya nyuma.”

 Katibu Mkuu huyo wa UNCTAD ameonya kuwa mikopo yoyote itumike ipasavyo ili iweze kuwa na manufaa kwa umma na hatimaye ilipwe kwa kipindi husika. Amesema kutokulipa madeni kuna athari kubwa na hata wakati mwingine kuweka rehani vizazi vijavyo an hivyo kuhatarisha ustawi wa nchi na hata kupoteza maendeleo yaliyokwishapatikana.