Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Kuwaelimisha watoto sasa kutazaa matunda katika vizazi vijavyo: Ban

Kuwaelimisha watoto sasa kutazaa matunda katika vizazi vijavyo: Ban

Wakati ulimwengu unakumbwa na uhaba wa fedha na rasilmali, viongozi wanatakiwa kuangazia elimu katika uwekezaji wa rasilmali hizo haba. Hiyo ni kauli ya Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki-moon, leo mjini Washington Marekani wakati wa mkutano wa kamati ya kwanza ya ngazi ya juu kuhusu mkakati wa kimataifa wa Elimu Kwanza, ambao ulizinduliwa mwezi Septemba mwaka 2012.

Akitoa mfano wa mtoto Malala Yousufzai, ambaye alishambuliwa na wanamgambo wa Taliban kwa sababu ya kupigia debe elimu ya mtoto wa kike, Bwana Ban amesema Umoja wa Mataifa unasimama bega kwa bega na Malala na mamilioni ya watoto wengine ambao wanastahili kupata elimu bora.

Bwana Ban ameelezea kufurahishwa na hatua zilizopigwa katika kufikia Lengo la Maendeleo la Milenia kuhusu Elimu, lakini ameongeza kuwa bado juhudi zaidi zinahitajika ili kupata matokeo mazuri zaidi.

(SAUTI YA BAN)

Tunaishi katika nyakati ngumu kifedha. Nyakati hizi zinahitaji uwekezaji wenye busara. Na hakuna uwekezaji wenye thamani zaidi ya elimu. Faida kubwa zaidi hutokana na kuwekeza katika wasichana na wanawake. Wakielimishwa, wanaweza kuchagiza maendeleo katika familia zao, jamii na mataifa. Tunastahili kuugeuza uelewa kuwa matokeo.”

Bwana Ban, ambaye pia amusisitiza ujumbe huo wakati wa mkutano wa mawaziri kutoka nchi nane zinazoangaziwa katika mkutano kuhusu hali ya elimu duniani, amesema anatumai kuwa kamati hiyo ya ngazi ya juu itabuni nafasi mwafaka ambazo zitaleta mabadiliko katika elimu chini ya mkakati wa Elimu Kwanza, ikiwemo kuwashawishi viongozi wa kimataifa kuunga mkono elimu.