Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Hali ya Syria ni janga la kibinadamu: OCHA

Hali ya Syria ni janga la kibinadamu: OCHA

Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa leo limejulishwa vile ambavyo wafanyakazi wa misaada wanakumbwa na vikwazo wanaposambaza misaada ya kibinadamu wananchi wa Syria walionaswa kwenye mgogoro wa kivita ambao shirika la Umoja wa Mataifa la kuratibu misaada ya kibinadamu, OCHA limeutia ni janga la kibinadamu.

Taarifa hiyo imewasilishwa na Mkuu wa OCHA Valerie Amos ambaye ametoa mfano kuwa msafara kutoka Damascus hadi Allepo unapita kilometa 210 lakini kuna vituo vya ukaguzi 50 huku wafanyakazi wakikabiliwa na hofu juu ya usalama wao.

(SAUTI YA AMOS)

“Sina jibu kwa Wasyria niliozungumza nao wakaniuliza mbona dunia imewatelekeza. Wakati hali ya kibinadamu ianzidi kuzorota, vikwazo tunavyokabiliana navyo vinafanya tukaribie kusitisha misaada muhimu ya kibinadamu. Tunafikia ukomo, Jumuiya ya kimataifa hususan wajumbe wa baraza hili washirikiane mara moja ili kuwasaidia wananchi wa Syria.”

Hata hivyo amewapongeza wafanyakazi wa misaada ambao licha ya hali mbaya ya usalama wameweza kupita maeneo hatarishi na kusambaza misaada muhimu kwa wakimbizi wa ndani na nje wa Syria.