Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Kuimarika kwa miundo mbinu mijini kutaboresha uchumi na mazingira UNEP

Kuimarika kwa miundo mbinu mijini kutaboresha uchumi na mazingira UNEP

Kuwekeza katika  miundombinu iliyo bora na teknolojia za kisasa vitatoa fursa nzuri ya kuwepo ukuaji wa uchumi mijini bila ya kuathiri mazingira, na hiyo ni  kwa mujibu wa ripoti ya Umoja wa Mataifa kuhusu miji katika nchi zinazoedelea.Inakadiriwa kuwa idadi ya watu wanaoishi mijini  itaongezeka kwa asilimia 70 ifikapo mwaka 2050.

Ripoti hiyo inapendekeza kupunguza matumizi ya  mafuta na kuanzisha matumizi ya nishati ya umeme kwenye sekta za usafiri mijini.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa ripoti hiyo mjini Nairobi Kenya, Mkurugenzi mkuu wa Shirika la mazingira la umoja wa Mataifa UNEP Achim Steiner  anasema kuwa ukuaji wa miji umekumbwa na matatizo ya kuzorota kwa mazingira na kuongezeka kwa maskini mijini.

 (SAUTI YA ACHIM)

“Miji haihusu tu miundo mbinu bali huduma , chakula , maji  kawi. Wakati ulimwengu ukitarajiwa kuwa na watu bilioni 9 ifikapo mwaka 2050 tutakuwa na uchafuzi , tutakuwa na maji machafu, tunakuwa na changamoto za usafi. Tumejifunza kuwa miji inaweza kuongeza matumizi ikiwa haitapangwa kutimiza malengo haya.”