Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Serry azungumzia kujiuzulu kwa Fayyad

Serry azungumzia kujiuzulu kwa Fayyad

Mratibu maalum wa Umoja wa Mataifa katika mchakato wa amani Mashariki ya Kati Robert Serry leo amekutana na Waziri Mkuu wa Palestina aliyejiuzulu Salam Fayyad, kumshukuru kwa niaba ya Umoja wa Mataifa kutokana na mafanikio yaliyopatikana wakati wa uongozi wake.

Bwana Serry amesema kiongozi huyo aliyejiuzulu sio tu kwamba amekuwa msuluhishi ambaye yeye anamheshimuwa kwa kiasi kikubwa bali pia mbia anayethaminiwa na jumuiya wa kimataifa ikiwemo Umoja wa Mataifa.

Amesema Umoja wa mataifa unatambua kuwa Waziri Mkuu Fayyad alijitahidi kukabiliana na vizingiti vya kufanikisha ajenda ya taifa la Palestina kwa kushirikiana na Rais Mahamud Abbas, ajenda ambayo amesema inakuwa hatarini iwapo kutakosekana kwa mazingira ya kisiasa ya kuaminika.

Hata hivyo amesema Umoja wa Mataifa utaendelea kushirikiana na wabia wa Palestina chini ya uongozi wa Rais Abbas ili kufikia maendeleo, kujenga nchi na kuafikia mashauriano yaliyodumu kwa muda mrefu ya kuwa ya suluhu ya mataifa mawili.