Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Maendeleo yapatikana katika kuepusha ukuaji wa kudumaa miongoni mwa watoto

Maendeleo yapatikana katika kuepusha ukuaji wa kudumaa miongoni mwa watoto

Ripoti mpya ya shirika la kuhudumia watoto duniani, UNICEF imeonyesha mafanikio katika harakati za kupunguza kudumaa miongoni mwa watoto walio na umri wa chini ya miaka mitano.Kudumaa kunakumba watoto Milioni 165 wenye umri huo na UNICEF inasema kuwa kuboresha lishe ndio suluhu pekee kama anavyoarifu George Njogopa.

(TAARIFA YA GEORGE)

Mkurugenzi Mtendaji wa UNICEF Anthony Lake amesema mtoto kudumaa katika makuzi kunaua fursa za maendeleo na uwezo wa ubongo kufikiri, na hivyo ushahidi wa mafanikio yaliyopatikana katika kuondoa tatizo hilo kumetoa changamoto ya kuongeza kasi.

Kwa mujibu wa ripoti hiyo mtoto mmoja kati ya watoto wanne wenye umri wa chini ya miaka mitano duniani amedumaa kutokana na unyafuzi na kwamba asilimia 80 ya watoto hao wako katika mataifa 14.

Hata hivyo UNICEF imesema nchi 11 zikiwemo Tanzania, Rwanda, Ethiopia na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo zimepiga hatua kwa kuboresha lishe kwa watoto na kuweka sera bora.