UNAMID yakaribisha makubaliano ya amani kati ya Sudan na JEM-Sudan
Mkuu mpya wa ujumbe wa pamoja wa Muungano wa Afrika na Umoja wa Mataifa Darfur (UNAMID) Mohamed Ibn Chambas, amekitaja kitendo cha kutiwa saini mkataba wa amani kati ya Sudan na kundi la Justice and Equality Movemnet (JEM-Sudan) kama hatua kubwa katika kutafuta amani Darfur.
Bwana Chambas amesema hayo mjini Doha, kufuatia hafla ya kutia saini mkataba huo ambao kwao JEM-Sudan linakuwa kundi la pili kuweka chini silaha na kufanya makubaliano ya amani na serikali ya Sudan, chini ya mkataba wa Doha kwa ajili ya amani Darfur (DDPD). Wa kwanza kufanya hivyo lilikuwa kundi la Liberation and Justice Movement lililosaini makubaliano ya amani mnamo Julai 14, 2011.
Bwana Chambas ameyasifu makubaliano hayo akiyataja kama yenye kuashiria ujasiri wa wahusika katika kuchagua njia ya mazungumzo na kulegeza misimamo mikali kwa ajili ya kulielekeza jimbo la Darfur kwenye suluhisho la mzozo ulowataabisha mno waathiriwa.