Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Shinikizo la damu tishio kwa nchi maskini na tajiri: Ban

Shinikizo la damu tishio kwa nchi maskini na tajiri: Ban

Wakati mataifa hii leo yanaadhimisha siku ya afya duniani, shinikizo la damu limetajwa kuwa chanzo cha magonjwa mengi yanayosababisha vifo duniani ambapo Katibu Mkuu Ban Ki-Moon amesema hali hiyo ya kiafya inakumba wakazi wa nchi maskini na nchi tajiri. Katika ujumbe wake, Bwana Ban amesema shinikizo la damu linatishia zaidi afya ya binadamu kwa kuwa inachukua muda mtu kubainika ana hali hiyo ya kiafya kwa sababu ni mara chache dalili kujitokeza. Hata hivyo amesema habari njema ni kwamba pindi mtu anabainika mapema kuwa na shinikizo la damu, kuna njia rahisi za kupambana nao ili kupunguza hatari ya kupata magonjwa ya moyo na kiharusi. Ametaja njia hizo kuwa ni pamoja na kupunguza matumizi ya chumvi iliyosindikwa, kufanya mazoezi, kuepuka msongo wa mawazo, kuacha kuvuta tumbaku na kuepuka unywaji pombe holela pamoja na kula mlo kamili. Shirika la afya duniani WHO linashauri kila mtu kupima kiwango cha mzunguko wa damu ili kuweza kuchukua hatua stahili.