Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Kikao cha tume ya kudhibiti silaha za nyuklia chaanza

Kikao cha tume ya kudhibiti silaha za nyuklia chaanza

Mwakilishi wa ngazi ya juu wa Umoja wa Mataifa kuhusu masuala ya kuondokana na silaha za nyuklia Angela Kane amezungumza katika kikao cha Tume ya kutokomeza silaha hizo na kusema ukosefu wa kuaminiana unakwamisha upatikanaji wa amani na ulinzi wa kudumu duniani.

Bi. Kane amesema hali hiyo ni jambo linaloibua mizozo Mashariki ya Kati, Asia ya Kusini na Kaskazini-Mashariki mwa Asia.

Amesema hali hiyo pia inatosha kuelezea kasi ndogo ya kufikia lengo la dunia la kuondokana na silaha za nyuklia na kuendelea kushamiri kwa mipango ya muda mrefu ya kuendeleza nyuklia.

Amewaambia wajumbe wa mkutano huo jambo hilo ni mzizi wa kura za mgawanyiko ndani ya baraza la usalama kuhusu masuala ya silaha pamoja na mkwamo wa mkutano wa mkataba wa kimataifa wa biashara ya silaha.

Amesema ni matumaini yake kuwa kikao cha tume hiyo kitakuwa na maafikiano mazuri kwa mwelekeo wa kupatia suluhu suala la kuendeleza silaha za nyuklia duniani.