Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Hali tete CAR: Ban, Baraza la Usalama watoa kauli

Hali tete CAR: Ban, Baraza la Usalama watoa kauli

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki Moon ameeleza kusikitishwa kwake na ripoti za kuendelea kwa mapigano huko Jamhuri ya Afrika ya Kati, CAR, licha ya makubaliano ya mwezi Januari mwaka huu yaliyoanzisha serikali ya Umoja wa kitaifa. Bwana Ban amekaririwa na msemaji wake akieleza kuwa mapigano yataongeza machungu na kutokuwepo na utulivu mambo yatakayokwamisha mchakato wa kufikia suluhu la kisiasa kwenye mzozo huo. Amesema ana nia ya kuzungumza na viongozi wa ukanda huo ili wawasihi wafanye lile wawezalo kusitisha mapigano na kushawishi pande husika kutekeleza makubaliano ya Libreville. Wakati huo huo, Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa baada ya kupokea taarifa ya hali halisi huko Jamhuri ya Afrika ya Kati kutoka kwa Naibu mkuu wa masuala ya siasa ndani ya umoja huo Taye-Brook Zerihoun, limetaka pande husika kuacha vitendo vya ukiukwaji wa haki za binadamu dhidi ya raia. Halikadhalika wametaka pande hizo kuruhusu mashirika ya misaada kusambaza misaada bila vikwazo vyovyote na kuzingatia makubaliano ya Libreville. Bwana Zerihoun alilieleza baraza hilo kuwa waasi wa Seleka sasa wanasonga kuelekea mji mkuu Bangui.