Jamii ya kimataifa yaombwa itafute suluhu la mzozo ulio nchini Syria.
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki-moon, amesema taifa la Syria kwa sasa linakabiliwa na hali ngumu ya kibinadamu huku zaidi ya watu milioni tatu wakilazimika kuhama makwao wakiwemo watu milioni moja wanaotafuta hifadhi katika nchi jirani.
Amesema kinachoshuhudiwa kufuatia hatua zilizochukuliwa na utawala wa Syria kupinga maandamano ya amani yaliyoanza miaka miwili ilopita ni cha kutia hofu, akitaja mashambulizi ya mabomu ya anga dhidi ya maeneo waliko raia, kuuawa kwa takriban watu 70,000 na ukiukaji mkubwa wa ubinadamu, na kutaka waliohusika kuchukuliwa hatua za kisheria.
Bwana Ban Ki moon ametoa wito kwa pande husika nchini Syria kutafuta suluhu la amani, na kuiomba jamii ya kimataifa, hususan Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kumuunga mkono mjumbe maalum Lakhdar Brahimi kuwasaidia watu wa Syria kupata suluhu la kisiasa la mzozo uliopo