Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Dunia yashindwa kukabiliana na mabadiliko ya mlo: FAO

Dunia yashindwa kukabiliana na mabadiliko ya mlo: FAO

Ukuaji wa uchumi, miji na mabadiliko mbali mbali duniani vimetajwa kusababisha mabadiliko ya mlo na mfumo wa maisha katika sehemu mbali mbali duniani huku serikali zikishindwa kukabiliana na mabadiliko hayo.  Hiyo ni kauli ya Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Chakula na kilimo duniani, FAO Jose Graziano da Silva aliyoitoa wakati akizungumza na wasomi katika chuo kikuu cha Wageningen, huko Uholanzi.  Bwana da Silva anasema hali hiyo inatokea wakati huu ambapo zaidi ya watu Milioni 870 wanakabiliwa na njaa ilhali wengine Milioni 500 wakikabiliawa na unene wa kupindukia unaowaweka hatarini kukumbwa na magonjwa yasiyoambukiza kama vile shinikizo la damu.  Amesema ni lazima kuweka mikakati ya kuhakikisha kunakuwepo na uzalishaji wa chakula salama na walaji wapatiwe taarifa sahihi na milo mbadala kwa afya bora. Mathalani, Bwana da Silva amesema kunahitajika mtazamo mpya kuhusu vyakula vya asili na dhima yake kwenye afya wakati huu ambapo vyakula hivyo vimepoteza nafasi yake kwenye milo ya kisasa.  Akiwa Uholanzi, Mkuu huyo wa FAO ametiliana saini makubaliano na chuo hicho kikuu ya kufanya tafiti za pamoja kuhusu masuala ya chakula.