Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Sasa ndio wakati wa kutimiza ahadi zetu kuhusu maendeleo: Ban

Sasa ndio wakati wa kutimiza ahadi zetu kuhusu maendeleo: Ban

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki-moon, amesema licha ya kupiga hatua katika kuboresha maisha ya watu, zaidi ya watu bilioni moja bado wanaishi katika umaskini ulokithiri.

Bwana Ban amesema hayo wakati wa kufungua kikao cha kundi la kuchukua hatua kuhusu Malengo ya Maendeleo Endelevu (SDGs), ambapo pia amesema uharibifu wa mazingira unaendelea kuhatarisha hali ya maisha ya kizazi cha sasa na vizazi vijavyo. Hata hivyo, Katibu Mkuu amesema bado kuna matumaini ya kutokomeza umaskini, kuwaletea mamilioni ya watu maji safi, mazingira safi na nishati safi.

Bwana Ban amesema Malengo ya Maendeleo ya Milenia ni na suluhu za mwongo uliopita zinaweza kuongoza katika mazungumzo ya sasa kuhusu kuendeleza malengo ya kiuchumi, kijamii na mazingira kwa njia jumuishi.

Katibu Mkuu ameongeza kuwa kasi ya kuyafikia malengo ya maendeleo ya milenia itaweza kutia moyo na kuchagiza uungwaji mkono wa ajenda ya maendeleo baada ya mwaka 2015. Amesema Umoja wa Mataifa pamoja na timu ya pamoja ya wataalam kutoka mashirika yote itakuwa tayari kutoa usaidizi wote unaofaa.