Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Ukata waiweka WFP katika hali ngumu, operesheni Syria mashakani

Ukata waiweka WFP katika hali ngumu, operesheni Syria mashakani

Shirika la mpango wa chakula duniani, WFP limesema linakabiliwa na changamoto kubwa ya kupanua wigo wa operesheni zake za dharura kwa ajili ya mamilioni ya watu walioko katika migogoro mbali mbali duniani.  Mkurugenzi Mtendaji wa WFP, Ertharin Cousin amesema wanakumbwa na hali hiyo ikiwemo ukata wakati huu ambapo Syria ambako nako wanapaswa kusaidia, mgogoro wake unaingia mwaka wa pili.  Amesema mgogoro wa Syria ni wa kidunia na hivyo wanahitaji mwitikio wa dunia nzima kuweza kukidhi mahitaji yanayoongezeka ya raia wa Syria.  Hata hivyo ametoa shukrani kwa misaada hadi sasa kutoka serikali 30 duniani ikiwemo Uingereza, Marekani na Umoja wa Ulaya huku akionya kuwa mahitaji yanaongezeka.  Bi. Cousin amesema WFP imepanga kuwafikia watu Milioni 2.5 nchini Syria huku akieleza kuwa zaidi  ya wasyria Milioni Moja walio nchi jirani maisha yao yako hatarini kutokana na uhaba wa rasilimali. WFP inahitaji dola Milioni 156 million za dharura ili kuweza kuendelea na operesheni zake za kupatia chakula raia wa Syria kuanzia sasa hadi mwezi Juni.