Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Ukatili dhidi ya wanawake hunipa uchungu: Ban

Ukatili dhidi ya wanawake hunipa uchungu: Ban

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki-moon, amesema ukatili dhidi ya wanawake na wasichana ni jambo ambalo humpa uchungu sana, akiongeza kuwa ndiyo maana amejitolea kuona kuwa mtandao wa viongozi wa kiume wanaopinga ukatili na kuwadhalimu wanawake unapanuka.

Akihutubia hafla ilofanyika pembezoni mwa mkutano wa tume inayohusika na masuala ya wanawake unaoendelea kwenye ukumbi wa Baraza Kuu, Bwana Ban amesema wanawake wanatakiwa kuishi bila uoga, huku wasichana wakifurahia haki yao ya kupata elimu kwa usalama.

Bwana Ban amesema Umoja wa Mataifa hauna budi kufanya kila liwezekanalo ili mambo haya yatimie katika maisha. Amesema wanawake wengi tu na wasichana hukumbwa na vitisho, pamoja na ukatili wa kimwili na kingono, hususan kutoka kwa watu wanaotakiwa kuwalinda zaidi, kama baba, waume zao, ndugu, walimu, wafanyakazi wenzao na hata wasimamizi wao.

Bwana Ban ameongeza kuwa tabia na mienendo inastahili kubadilishwa, pamoja na sheria kubadilishwa na kutekelezwa, ili wanaotenda ukatili huo wafikishwe mbele ya sheria.