Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Ukoloni hauna nafasi katika ulimwengu wa sasa: Ban

Ukoloni hauna nafasi katika ulimwengu wa sasa: Ban

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki-moon, ameiambia kamati maalum kuhusu kutokomeza ukoloni kwamba, sasa ndio wakati wa kuwa na ya aina mpya ya mazungumzo kuhusu ukoloni, na ambayo yanawajumuisha wote.

Bwana Ban amesema kuwa jamii ya kimataifa sasa inashikilia hata zaidi dhana kuwa, ukoloni hauna nafasi katika ulimwengu wa sasa.

Katibu Mkuu ameongeza kuwa, kutokomeza ukoloni kwa kushikilia kanuni za mkataba mkuu wa Umoja wa Mataifa, pamoja na maazimio husika ya Umoja wa Mataifa ni jukumu la kila mmoja, na ambalo linahitaji ujumuishwaji wa wote. Amesema kamati hiyo maalum inafaa kuwa mstari wa mbele katika kutambua nafasi za mabadiliko na kuendeleza masuala muhimu katika harakati za kutokomeza ukoloni.

“Kama kamati ya kimataifa iliyo na jukumu la kutokomeza ukoloni, kamati hii inastahili kubuni njia mpya na za kistadi ili kuchagiza ari ya kisiasa ya kuendeleza ajenda hii. Kama tunavyojua, ulimwengu upo katika wakati wa mabadiliko. Mifumo mingi ya kijadi inavunjwa sasa. Mifumo mipya inawekwa. Katika uwanja wa ukoloni, maeneo 16 yasiyo huru yanahitaji uzingativu wetu.”

(SAUTI YA BAN Duration:  33″)

Bwana Ban amesema kwamba sasa ndio wakati wa kuchukuwa hatua na kutekeleza mambo ili kuona matunda, na wala sio wakati wa kuahirisha mambo, huku ikiendelezwa desturi ya kuongea tu.