Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Ban akutana na waziri mpya wa mambo ya nje Marekani, John Kerry

Ban akutana na waziri mpya wa mambo ya nje Marekani, John Kerry

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki-moon, leo amekutana na kufanya mashauriano na Waziri mpya wa Mambo ya nje wa Marekani, John Kerry. Wakizungumza na waandishi wa habari mjini Washington, Marekani, Bwana Ban amempongeza Bwana Kerry kwa uteuzi wake katika wadhfa huo, na kumsifu kwa ushirikiano wake kuhusu masuala mengi, yakiwemo ya kisiasa, usalama na ongezeko la joto duniani.

Bwana Ban ametoa wito kwa serikali ya Marekani iendelee kuongoza katika kukabiliana na changamoto nyingi za kikanda na kimataifa. Viongozi hao wawili wamejadili masuala kadhaa, yakiwemo mizozo ya Syria na Mali.

Pamoja na hayo, Bwana Ban amesema jaribio la zana za nyuklia lililofanywa na Jamhuri ya Korea Kaskazini ni uchokozi wa moja kwa moja dhidi ya jamii ya kimataifa, akiongeza kuwa mara kwa mara ametoa wito kwa serikali ya Korea Kaskazini kukomesha mipango yake ya nyuklia na badala yake kuzingatia masuala ya hali ya kibinadamu na haki za binadamu nchini humo. Amesema kuwa ameliomba Baraza la Usalama kuchukua hatua ya pamoja haraka iwezekanavyo, akisema anatarajia ushirikiano wa Bwana Kerry wa hilo.

Masuala mengine waliyojadili ni lile la nyuklia Iran, amani ya Mashariki ya Kati, masuala ya maendeleo endelevu, pamoja na kampeni ya kupinga dhuluma dhidi ya wanawake ya One Billion Rising.