Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Mikopo kwa mangariba yaokoa afya ya wanawake na watoto wa kike

Mikopo kwa mangariba yaokoa afya ya wanawake na watoto wa kike

Siku ya Jumatano ya tarehe Sita mwezi Februari mwaka huu wa 2013, dunia ilipata fursa ya kutathmini harakati za kutokomeza ukeketaji wa watoto wa kike na wanawake, FGM. Siku hiyo ilikuwa ni fursa maalum kwa kuwa ni siku ya kimataifa ya kutokomeza ukeketaji wanawake na watoto kama ilivyopitishwa na Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa mwezi Disemba mwaka jana.

Katika tathmini ya siku hiyo, ilielezwa kuwa kwa sasa hatari ya watoto wa kike wenye umri wa kati ya miaka 15 hadi 19 kufanyiwa kitendo hicho dhalili ni ndogo zaidi ikilinganishwa na ilivyokuwa kwa wanawake ambao kwa sasa wana umri wa kati ya miaka 45 – 49. Na zaidi ya hapo ilielezwa kuwa kutokana na mafanikio hayo yaliyosababishwa na elimu zaidi ya athari za vitendo hivyo, FGM sasa yafanyika kwa siri zaidi na hivyo kutoa changamoto zaidi kwa harakati za kutokomeza vitendo hivyo. Je nini kimefanyika? Ungana na Assumpta Massoi katika makala haya.