Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Feltman apongeza mchango wa Burundi nchini Somalia

Feltman apongeza mchango wa Burundi nchini Somalia

Msimamizi Mkuu wa masuala ya kisiasa ndani ya Umoja wa Mataifa Jeffrey Feltman amehitimisha ziara yake nchini Burundi na kupongeza mchango wa nchi hiyo katika ujenzi wa amani na utulivu nchini Somalia.

Feltman amesema hayo alipozungumza na waandishi wa habari mjini Gitega nchini Burundi baada ya mazungumzo yake na Rais wa nchi hiyo Pierre Nkurunziza.

Amesema wananchi wa Somalia kwa sasa wana matumaini na hatma ya nchi yao kutokana na kujitoa kwa hali na mali kulikofanywa na Burundi na nchi nyingine jirani kwa lengo la kuona amani na utulivu vinarejea Somalia.

Halikadhalika Feltman amesema Umoja wa Mataifa unashukuru kwa ahadi iliyotolewa na Burundi ya kusaidia wananchi wa Mali.

Naye Rais Nkurunziza amesema baada ya nchi yao kupata msaada wa hali na mali kutoka Umoja wa Afrika na Umoja wa Mataifa, sasa Burundi  inawajibika kusaidia wengine kwa lengo la kujenga amani na utulivu duniani