Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Bado hatujaweza kufikia maeneo yote Syria: OCHA

Bado hatujaweza kufikia maeneo yote Syria: OCHA

Mkuu wa operesheni katika Shirika la Umoja wa Mataifa la misaada ya kibinadamu,  OCHA, John Ging amesema hali  ya Syria bado inazidi kudorora kadri siku zinavyosonga na kwamba bado hawajapata kibali cha kuweza kuvuka eneo la mzozo na kuwafikia awle wote wanaohitaji misaada.

Bwana Ging amewaambia waandishi wa habari mjini New York, Marekani kuwa wakati wa ziara yao ya siku nne nchini Syria  waliweza kujionea hali halisi ya madhila ya wananchi wa Syria na kuzungumza na mamlaka husika ili kuweza kuvuka mpaka wa mzozo lakini japo kuna mafanikio lakini bado haitoshi.

(SAUTI YA Ging)

“Kuweza kuvuka na kuingia upande wa pili wa mzozo ni changamoto ya kila siku kwa washirika wetu wa kutoa msaada. Baada ya mashauriano na serikali  walikubali kwa mtazamo wao kuwa tunaweza kupata msaada wowote tunaohitaji ili tuweze kuingia upande wa pili wa mgogoro. Tufanya majaribio tulipoenda Homs na tuliweza kuingia vizuri Talbese. Kama watoa msaada tunatafuta fursa ya kuweza kufikia maeneo yote. Tumesema bayana kuwa kwa kuzingatia mpango wa sasa wa kufikia maeneo hayo hatutaweza kufikia baadhi ya maeneo yanayokaliwa na wapinzani huko Kaskazini.”

Bwana Ging amesema pamoja  na vikwazo hivyo bado pia uhaba wa fedha unawakabili kuweza kukidhi mahitaji na hivyo ni matumaini yake kuwa mkutano wa wahisani wa Syria utakaofanyiak Kuwait utatoa majibu ya changamoto nyingi zinazowapata.

OCHA inasema kwa sasa zaidi ya watu Milioni Mbili ni wakimbizi wa ndani nchini Syria huku Milioni Nne wakihitaji misaada ya kibinadamu na familia zao zimetindikiwa uwezo wa kuwasaidia.