Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Bara la Afrika linasonga mbele: Ban

Bara la Afrika linasonga mbele: Ban

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-Moon ameunga mkono maendeleo barani Afrika ikiwemo masuala ya utawala bora na haki za binadamu ambapo amesema mtazamo wake ni kwamba bara hilo linaibuka na kusonga mbele.

Akizungumza na waandishi wa habari mjini Addis Ababa, Ethiopia, Bwana Ban ametoa mfano wa harakati za Afrika za kupambana na magonjwa kama vile Ukimwi, Malaria na vifo vya wajawazito na watoto wachanga ambapo amesema ikiwa zimebakia siku Elfu Moja kufikia ukomo wa malengo ya maendeleo ya Milenia, juhudi zaidi zahitajika na hatua iliyofikiwa ni fursa ya kutumia.

Halikadhalika amegusia ukatili wa kingono kwenye migogoro na kutaka viongozi wa Afrika waungane naye kupaza sauti kwa niaba ya waathirika wa vitendo hivyo ambavyo bado vinagubikwa na ukimya.

Bwana Ban pia amezungumzia utiaji saini kwa mpango wa kisiasa wa Jamhuri ya kidemokrasi ya Congo uliokuwa ufanyike leo lakini umeahirishwa kutokana na kuibuka kwa tofauti za kimsingi.