Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

UM waonya kuhusu kuajiri watoto katika vita Jamhuri ya Afrika ya Kati

UM waonya kuhusu kuajiri watoto katika vita Jamhuri ya Afrika ya Kati

Mwakilishi maalum wa Umoja wa Mataifa kuhusu watoto na vita vya silaha, Bi Leila Zerrougui, ameelezea kusikitishwa kwake na ripoti za hivi karibuni kuhusu kuajiriwa kwa watoto na makundi yenye silaha yanayojumuisha muungano wa waasi wa Seleka katika Jamhuri ya Afrika ya Kati.

Akilihutubia Kundi la kuchukua hatua la Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa mnamo siku ya Ijumaa, Bi Zerrougui amekaribisha mikataba ya amani ilosainiwa baina ya serikali, muungano wa Seleka, makundi ya kisiasa na kijeshi, pamoja na vyama vya kisiasa mjini Libreville, huku akilitahadharisha kundi hilo la Umoja wa Mataifa kuhusu kuajiriwa kwa watoto kunakoendelea.

Bi Zerrougui amesema ripoti za kuajiri watoto katika vita vya silaha ni kinyume na mahakikisho yalotolewa na makundi ya Seleka, na ni lazima kukome mara moja. Mwakilishi huyo maalum pia ameelezea wasiwasi kuhusu kujitolea kwa serikali ya Jamhuri ya Afrika ya Kati kuwalinda watoto, huku akisema aanasikitishwa na hali ya ukiukaji wa haki za watoto ambao umekuwa ukiendelea kwa muda mrefu.