Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Ujumbe wa Umoja wa Mataifa waenda Mali

Ujumbe wa Umoja wa Mataifa waenda Mali

Ujumbe wa Umoja wa Mataifa unawasili Mali hii leo kusaidia serikali ya nchi hiyo kurejesha utulivu na utangamano.

Msemaji wa Umoja huo Martin Nesirky amesema ujumbe huo wa awali unaongozwa na Joao Honwana kutoka Idara ya masuala ya kisiasa ya Umoja wa Mataifa na jukumu lao ni kushirikiana na serikali ya Mali katika kutekeleza azimio 2085 la Baraza la Usalama.

Azimio hilo lililopitishwa mwezi uliopita linahusisha kupelekwa kwa jeshi la Afrika litakalopata usaidizi wa kimataifa, AFISMA kwa kipindi cha awali cha mwaka mmoja na pia kuanzisha ofisi ya Umoja wa Mataifa huko Mali itakayojikita na masuala mbali mbali.

Tayari imeripotiwa kuwa Said Djinnit ambaye ni mwakilishi maalum wa Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa amekuwa na mazungumzo na Rais Dioncounda TRaore wa Mali mjini Bamako ambako pia atashiriki mkutano wa wakuu wa ECOWAS.