Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

ICC sasa yamulika uhalifu wa kivita Mali

ICC sasa yamulika uhalifu wa kivita Mali

Mwendesha mashtaka Mkuu wa Mahakama ya kimataifa ya makosa ya jinai yanayohusika na uhalifu wa kivita, ICC, Fatou Bensouda amefungua rasmi uchunguzi dhidi ya vitendo vya  uhalifu vinavyodaiwa kufanyika Mali tangu mwezi Januari mwaka jana.

Hatua hiyo inafuatia uchunguzi wa awali uliofanywa na ofisi yake kuhusu hali halisi nchini Mali ambapo sasa amesema ameridhika kuwa vigezo vya kisheria vimekamilika na uchunguzi usio na upendeleo wowote unaanza kwa maslahi ya raia wa nchi hiyo.

Bensouda amesema tangu kuanza kwa mapigano mwezi Januari mwaka jana wakazi wa Mali kaskazini wamekuwa wakiishi katika mazingira ya mateso wakifanyiwa vitendo dhalimu na vikundi vyenye silaha.

Uchunguzi huo dhidi ya vitendo kama vile mauaji, utesaji na ubakaji vinavyotambuliwa kuwa ni uhalifu wa kivita kwa mujibu wa katiba inayoanzisha mahakama hiyo utafanyika katia mikoa mitatu ya kaskazini mwa Mali.