Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Wasyria kuweni macho mgogoro unararua Taifa: Ban

Wasyria kuweni macho mgogoro unararua Taifa: Ban

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-Moon amewataka wananchi wa Syria kutafakari upya mgogoro unaondelea nchini mwao ambao amesema unazidi kurarua taifa hilo vipande vipande.

Bwana Ban amesema hayo katika taarifa iliyomnukuu kufuatia shambulio dhidi ya Chuo Kikuu Aleppo kwenye mji wa Aleppo nchini Syria ambapo watu zaidi ya 80 wameripotiwa kuuawa na wengi wengi wamejeruhiwa.

Pamoja na kusikitishwa kwake na tukio hilo na kutuma rambirambi kwa familia za wahanga, Bwana Ban amelaani shambulio dhidi ya raia amblo amesema ni kitendo cha kinyama na kutaka pande zote husika kuzingatia sheria za kimataifa kuhusu haki za binadamu.

Ametaka suluhisho la amani dhidi ya mzozo huo, suluhisho ambalo amesema linapaswa kuzingatia matakwa ya demokrasia ya wananchi wa Syria.