Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Kurejea kwa Dkt. Mukwege ni ujasiri: Meece

Kurejea kwa Dkt. Mukwege ni ujasiri: Meece

Mwakilishi maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa huko Jamhuri ya kidemokrasi ya Congo, DRC, Roger Meece ameunga mkono kurejea huko Bukavu, Kivu Kusini kwa Dkt. Denis Mukwege, Mganga Mkuu wa hospitali ya Panzi ambaye mchango wake kwa tiba kwa wanawake waliokumbwa na ukatili wa kingono ikiwemo kubakwa unatambulika duniani kote.

Bwana Meece ambaye ni mkuu wa MONUSCO amesema kitendo cha kijasiri cha Dkt. Mukwege  kurejea licha ya kushambuliwa nyumbani kwake mwezi Oktoba mwaka 2012 kinadhihirisha utayari wake wa kusaidia wanawake hao.

Amesema ni matumaini yake kuwa taarifa kuhusu shambulio hilo zitawekwa wazi na wahusika kuwajibishwa na kwamba MONUSCO itasaidia mamlaka za Kivu Kusini kumpatia usalama anaohitaji Dkt. Mukwege ili aweze kutekeleza kazi zake.