Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Ban apongeza mpango wa mkutano wa Bashir na Kiir

Ban apongeza mpango wa mkutano wa Bashir na Kiir

Marais Omar Al Bashir wa Sudan na Salva Kiir wa Sudan Kusini Ijumaa watakuwa an mazungumzo yanayoratibiwa na Umoja wa Afrika kupitia Rais wa zamani wa Afrika Kusini Thabo Mbeki.

Mazungumzo hayo yatafanyika nchini Ethiopia chini ya wenyeji wa Waziri Mkuu uwa nchi hiyo Hailemariam Desalegn ambapo Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-Moon ameunga mkono mpango huo wa mazungumzo.

Taarifa ya msemaji wa Bwana Ban, imemkariri Katibu Mkuu huyo akiwasihi Bwana Al Bashir na Bwana Kiir kutoa maamuzi kuhusu masuala ambayo bado hayajapatiwa ufumbuzi ikiwemo mzozo wa mpaka kati ya nchi zao, usalama na hatma ya jimbo la Abyei. Pia amewakumbusha watekeleze makubaliano yote yaliyotiwa saini tarehe 27 mwezi Septemba mwaka jana kuhusiana na nchi mbili hizo.

Bwana Ban amesema Umoja wa Mataifa kwa upande wake uko tayari kusaidia pande zote kutekeleza makubaliano yao na suluhisho la migogoro ambayo bado haijatatuliwa.