Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Jeshi la Sudan ladaiwa kufanya mashambulizi ya anga, raia wakimbia: UNAMID

Jeshi la Sudan ladaiwa kufanya mashambulizi ya anga, raia wakimbia: UNAMID

Ujumbe wa pamoja wa Umoja wa Mataifa na Umoja wa Afrika unaolinda amani kwenye jimbo la Darfur, nchini Sudan UNAMID, umeeleza wasiwasi wake juu ya ripoti za raia kukimbia makazi yao kutokana na mashambulio ya anga yanayodaiwa kufanywa na jeshi la Sudan na vikundi vyenye silaha huko Shangil Tobaya na Tawila kaskazini mwa Darfur.

Taarifa iliyotolewa na Ofisi ya msemaji wa Umoja wa Mataifa UNAMID ilituma kikosi chake cha doria siku ya Jumatano kwenda Shanghil Tobaya lakini jeshi la Sudan lilizuia wasiingie eneo hilo.

Halikadhalika imesema kuwa mapigano ya tarehe 12 mwezi huu kati ya jeshi la Sudan na kundi la wapiganaji lisilofahamika karibu na eneo hilo yalisababisha kifo cha mpiganaji mmoja na kujeruhiwa raia wawili.

UNAMID imesema inajipanga kuchunguza matukio hayo na mengine huku ikitaka pande zinazozozana kuacha mapigano kwani wanaoumia ni raia hususan wale wanaoishi katika kambi.