Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

WFP kutoa mgao wa dharura wa chakula huko Yarmouk: Yahitaji fedha zaidi

WFP kutoa mgao wa dharura wa chakula huko Yarmouk: Yahitaji fedha zaidi

Shirika la mpango wa chakula la Umoja wa Mataifa, WFP litaanza kusambaza msaada wa dharura wa chakula kwa maelfu ya wakimbizi wa kipalestina waliokumbwa na mapigano kwenye kambi ya Yarmouk, iliyoko mji mkuu wa Syria, Damascus.

WFP inatarajia kuwapatia msaada huo ambao ni mlo wakimbizi 125,000 wa kipalestina pamoja na raia wa Syria waliokimbia makazi yao.

Kambi ya Yarmouk yenye idadi kubwa ya wakimbizi wa Kipalestina wiki hii ilikuwa eneo la mapigano makali yaliyosababisha takribani wakimbizi Laki Moja wa kipalestina kukimbia.

Hata hivyo WFP imesema operesheni hiyo ya dharura inahitaji nyongeza ya dola Milioni Moja na Nusu ili kununua tani 580 zaidi za chakula kwa ajili ya kipindi cha miezi mitatu ijayo. Elisabeth Byrs ni msemaji wa WFP mjini Geneva.

Usambazaji utaanza siku chache zijazo na kila familia itapatiwa kilo 12 za vyakula vya kwenye makopo vilivyo tayari kuliwa kila wiki. Wakimbizi wa kipalestina na maelfu ya wasyria waliokimbia makwao walijihifadhi kwenye kambi hiyo na baadaye walikimbia kutokana na kuongezeka kwa mapigano. Hivi sasa wengi wanaishi na jamaa zao. Wengine wanaishi kwenye misikiti, shule. Wanakabiliwa na baridi, wana hofu. Sisi tutajitahidi kuwafikia hao wanaojulikana waliko kwenye majengo ya umma na kuwapatia mgao wa chakula.”