Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

UM wataka kurejeshwa haraka kwa mchakato wa amani kati ya Israeli na Palestina

UM wataka kurejeshwa haraka kwa mchakato wa amani kati ya Israeli na Palestina

Wito wa kutaka kurejeshwa kwa haraka mchakato wa amani kati ya Palestina na Israeli umetolewa kwa nyakati tofauti hii leo kwenye makao makuu ya Umoja wa Mataifa mjini New York, Marekani, kutokana na mazungumzo ya moja kwa moja kati ya pande mbili hizo kufanyika mara ya mwisho mwezi Septemba mwaka 2010.

Katika mkutano wake wa mwisho wa mwaka na waandishi wa habari Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-Moon amesema mchakato huo umekumbwa na mkwamo na pande hizo zimekuwa na mvutano mkubwa ambao haujawahi kutokea.

Bwana Ban amesema pamoja na kwamba mapigano yamesitishwa huko Ukanda wa Gaza, ni dhahiri kuwa amani ni zaidi  ya mazingira ya kutokuwepo kwa vita.

Naye msimamizi mkuu wa masuala ya siasa katika Umoja wa Mataifa Jeffrey Feltman, amelieleza Baraza la Usalama kuwa ujenzi wa makazi ya walowezi huko Ukingo wa Magharibi mwa mto Jordan ambao unafanywa na Israeli ni kinyume na sheria za kimataifa na unahatarisha mipango yote ya amani Mashariki ya Kati.