Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Haki za wahamiaji zilindwe: Jopo la wataalamu wa haki

Haki za wahamiaji zilindwe: Jopo la wataalamu wa haki

Jopo la wataalamu wa haki za binadamu kutoka Umoja wa Mataifa, Umoja wa Afrika, wataalamu wa haki za wahamiaji na Muungano wa nchi za bara la Amerika limeelezea wasiwasi wake kuhusu tabia ya baadhi ya nchi kuchukulia kitendo cha mtu kukosa nyaraka rasmi za ukaazi kama uhalifu.

Katika taarifa ya pamoja kuadhimisha siku ya kimataifa ya wahamiaji hii leo, jopo hilo limesema kuvuka mipaka bila nyaraka muhimu, kuzididisha muda wa ukaazi katika nchi bila nyaraka siyo kosa la uhalifu moja kwa moja bali ni kosa la kiutawala.

Wamesema haki ya binadamu inatokana na utu wa mtu na siyo utaifa au hadhi ya uhamiaji.

Wataalamu hao pia wametaka dunia itambue mchango unaotolewa kila siku na mamilioni ya wahamiaji duniani katika kuboresha maisha ya kila mkazi wa dunia.

Kutokana na hali hiyo wametaka nchi kuridhia mikataba ya kimataifa ya haki za binadamu ikiwemo ule wa kimataifa wa ulinzi wa haki za wahamiaji na familia zao.