Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Ukarabati jengo la UM wachangia kupunguza uchafuzi wa mazingira: Ban

Ukarabati jengo la UM wachangia kupunguza uchafuzi wa mazingira: Ban

Hatimaye Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-Moon amerejea katika ofisi yake iliyoko kwenye jengo kuu la umoja huo mjini New York, Marekani baada ya ukarabati uliodumu kwa takribani miaka mitano.

Akizungumza na waandishi wa habari baada ya kuingia katika ofisi yake hiyo, Bwana Ban amesema ukarabati huo ni wa kihistoria kwa kuwa umezingatia uhifadhi wa mazingira.

Ninatoa shukrani za dhati kwa nchi zote wanachama. Kwa ukarabati huu naamini tunaweza kuhudumia vizuri zaidi watu duniani kote. Kitendo cha leo ni hatua kubwa kwa sura mpya ya sekretarieti ya Umoja wa Mataifa. Kama unavyofahamu umoja wa Mataifa umekuwa ukiongoza kwa mifano suala la maendeleo endelevu. Kwa ukarabati huu tumepungzua angalau kwa asilimia 50 matumizi ya nishati na maji na pia asilimia 40 uzalishaji wa hewa ya ukaa. Na bila shaka tutaendelea kuboresha zaidi.”

Bwana Ban amesema licha ya uhaba wa fedha, nchi wanachama ziliridhia ukarabati wa majengo hayo na ameshukuru pia Marekani ambayo ni mwenyeji wa makazi ya Umoja wa Mataifa kwa kuvumilia ukarabati.

Majengo ya makao makuu ya Umoja wa Mataifa yalijengwa kati ya mwaka 1950 na 1952 yamechoka na ukarabati huo ulioanza miaka mitano iliyopita unatarajiwa kukamilika mwaka 2014.