Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Mjadala wa kitaifa ufanyike haraka Mali ili kuepusha mizozo: Ban

Mjadala wa kitaifa ufanyike haraka Mali ili kuepusha mizozo: Ban

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-Moon amesema anakwazika na mazingira yaliyosababisha kujiuzulu kwa Waziri Mkuu wa Mali, Cheick Modibo Diarra huku akitaka jeshi liache kuingilia masuala ya kisiasa na uongozi wa Mali umalize mivutano yote kwa njia ya amani.Bwana Ban amekaririwa na msemaji wake akieleza kuwa matukio ya hivi karibuni huko Mali yanaonyesha umuhimu wa jitihada za kitaifa na kimataifa za kushughulikia mzozo wa kisiasa nchini humo.

Amemsihi Rais wa serikali ya mpito nchini Mali Dioncounda Traore, kuanzisha haraka mashauriano ya uteuzi wa Waziri Mkuu anayekubalika na pande zote na kuunda serikali jumuishi.

Bwana Ban amesema ni vyema mchakato huo ukafanyika haraka pamoja na mjadala wa kitaifa wa kuamua mwelekeo wa kipindi cha mpito ikiwemo kufanyika kwa uchaguzi na kurejesha utawala wa kikatiba.