Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Baraza Kuu la UM laadhimisha miaka 30 ya mkataba kuhusu sheria ya bahari

Baraza Kuu la UM laadhimisha miaka 30 ya mkataba kuhusu sheria ya bahari

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki- Moon ametaka kuongezwa kwa shime zaidi duniani ili nchi zote zitie saini na kuridhia mktaba wa kimataifa wa sheria ya bahari, ambao mara nyingi hutambuliwa kama Katiba ya masuala ya bahari.

Akihutubia Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa katika maadhimisho ya miaka 30 tangu kupitishwa kwa mkataba huo, Bwana Ban amesema mkataba huo kama ilivyo kwa katiba, ni msingi thabiti unaotoa maelekezo, mwongozo, utulivu na utabiri kwa misingi ya sheria.

Licha ya kueleza kuhamasika na idadi ya nchi wanachama katika mkataba huo ambazo ni 163 na Umoja wa Ulaya, ametaka hatua zaidi ili nchi zote ziridhie kutetea na kulinda mkataba huo wa sheria ya bahari uliopitishwa na baraza hilo mwaka 1982.

Naye Rais wa mkutano wa Tatu wa Umoja wa Mataifa khus sheria ya Bahari, Tommy Koh amesema ni jambo la kushangaza watu wanafahamu zaidi kuhusu anga na kusahau masuala ya bahari ambaye amefananisha kama mapafu ya sayari ya dunia.

Ameliezea Baraza hilo Kuu la Umoja wa Mataifa kuwa ni vyema elimu zaidi kuhusu masuala ya bahari na udhibiti wake ikatolewa kwa kuwa madhara ya ongezeko la joto duniani ni kuongezeka kwa kiwango cha maji ya bahari, hali inayoweza kufanya baadhi ya visiwa kumezwa na maji.