Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Awamu ya pili ya kampeni ya chanjo ya Homa ya Manjano kuanza mwezi huu Darfur

Awamu ya pili ya kampeni ya chanjo ya Homa ya Manjano kuanza mwezi huu Darfur

Awamu ya pili ya chanjo dhidi ya ugonjwa wa homa ya manjano huko Darfur nchini Sudan inatarajiwa kuanza mwezi huu ili kudhibiti ugonjwa huo uliolipuka mwezi Septemba mwaka huu ambapo watu 165 wameshakufa kutokana na ugonjwa huo huku 732 wakishukiwa kuugua kwenye vitongoji 33 kati ya 64 vya jimbo la Darfur.

Wizara ya afya ya Sudan inaratibu awamu hiyo kubwa ya pili ya kampeni ya chanjo kwa ajili ya watu Milioni Moja na Laki Mbili ambapo awamu ya kwnza iliyoanza tarehe 21 mwezi uliopita inafikia watu Milioni Mbili na Laki Mbili.

Kampeni ya chanjo inafadhiliwa na vikundi kadhaa ikiwemo kikundi cha kimataifa cha chanjo dhidi ya homa ya manjano, Ushirikiano wa kimatafa kwa chanjo-GAVI, Umoja wa Ulaya na mashirika ya kiraia ambako chanjo hiyo inatolewa.

Tayari shirika la afya duniani WHO limeweka hadhari ya mlipuko wa ugonjwa huo na linaongeza wataalamu zaidi kusaidia harakati za serikali ya Sudan za kudhibiti ugonjwa huo.