Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Mpango wa Jamhuri ya kidemokrasia ya watu wa Korea kurusha roketi watia wasiwasi: Ban

Mpango wa Jamhuri ya kidemokrasia ya watu wa Korea kurusha roketi watia wasiwasi: Ban

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-Moon ameonyesha wasiwasi mkubwa juu ya mpango wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya watu wa Korea, DPRK ya kutaka kurusha roketi kwenda anga za juu na kuitaka nchi hiyo kufikiria upya uamuzi wake ikiwemo kusitisha kabisa shughuli hiyo.

Msemaji wa Bwana Ban, amemkariri Katibu Mkuu huyo wa Umoja wa Mataifa akisema kuwa uzinduzi wa wowote wa roketi ni kinyume na azimio namba 1874 la Baraza la Usalama ambalo linaitaka DPRK kutofanya uzinduzi wowote unaotumia teknolojia ya makombora ya masafa marefuu.

Amesema kitendo hicho kikitekelezwa kitaongeza wasiwasi katika eneo la rasi ya Korea na Asia kwa ujumla.

Jumamosi iliyopita DPRK ilikaririwa kutangaza kuwa kati ya tarehe 10 na 22 mwezi huu itafanya jaribio la kupeleka setilaiti anga za juu . Jaribio kama hilo lilifanyika mwezi Aprili mwaka huuu lakini halikufanikiwa.