Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Juhudi za wanawake za kuendeleza amani na usalama zinapaswa kuungwa mkono: UM

Juhudi za wanawake za kuendeleza amani na usalama zinapaswa kuungwa mkono: UM

Mkuu wa shirika la Umoja wa Mataifa linalohusika na masuala ya wanawake, UN-WOMEN Michelle Bachelet amesema michango ya mashirika ya wanawake na makundi ya kiraia ya kuzuia na kutatua migogoro duniani ni muhimu katika kuleta amani duniani na hivyo jitihada hizo zinapaswa kuungwa mkono.

Amesema hayo wakati akiwasilisha ripoti ya Katibu Mkuu wa umoja wa Mataifa, kuhusu wanawake, amani na usalama, ripoti aliyowasilisha wakati wa mjadala wa wazi wa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa mjini New York, Marekani.

Bi. Bachelet ametoa mfano wa Mali ambako amesema vikundi vya wanawake vinashiriki ipasavyo kutumai njia salama kumaliza mgogoro kwenye nchi hiyo ambayo imegawanyika tangu waasi wadhibiti eneo la kaskazini mapema mwaka huu.

Amesema licha ya kwamba wanawake hao hawajashirikishwa rasmi katika mchakato wa amani nchini mwao, viongozi wanawake kaskazini mwa Mali wanatumia mbinu zao kuwataka viongozi wa vikundi vyenye silaha kushiriki katika mashauriano ya amani.

Bi. Bachelet amesema dunia inapaswa kuhakikisha wanawake wana fursa zote za kutekeleza majukumu yao ya katika kulinda amani na usalama.