Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Mkutano kuhusu amani na utulivu kama msingi wa dira ya maendeleo duniani kufanyika Liberia

Mkutano kuhusu amani na utulivu kama msingi wa dira ya maendeleo duniani kufanyika Liberia

Majanga na mizozo ya kivita ambayo huathiri zaidi ya watu milioni 200 na kusababisha vifo vya watu zaidi la laki tano duniani kote itakuwa ajenda kuu ya mkutano unaoanza kesho nchini Liberia kuhusu migogoro na hatari za kutumbukia kwenye mizozo .

Kongamano hilo likiwa linajikita zaidi kwa bara la Afrika, limeandaliwa kwa ushirikiano kati ya serikali ya Liberia na Finland na washiriki wanatoka sekta mbali mbali ikiwemo serikalini, taasisi za kiraia, viongozi wa kijadi, vyombo vya habari na vyama vya wafanyakazi.

Judy Cheng-Hopkins ambaye ni msaidizi wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa kwa masuala ya ulinzi wa amani amesema mizozo yenye ghasia imekumba watu wengi sehemu mbali mbali duniani hivyo ni vyema viongozi wa dunia kupitia kongamano hilo nao wakapata uelewa na kushiriki katika mchakato wa kukabiliana na hali hiyo.

Umoja wa Mataifa unasema unatambua kuwa migogoro, ghasia na majanga ni vikwazo dhahiri vya kutimiza malengo ya maendeleo ya milenia kwa nchi nyingi zinazoendelea na kwamba kongamano ni mfululizo wa mashauriano yanayoongozwa na umoja wa mataifa wa kupata maoni jinsi masuala ya majanga, mizozo na usalama wa raia yanaweza kujumuishwa katika mpango mpya wa dunia wa maendeleo baada ya 2015.