Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Ongezeko la joto duniani huenda likawa juu zaidi udongo wenye barafu ukiyeyuka kwa kasi: UNEP

Ongezeko la joto duniani huenda likawa juu zaidi udongo wenye barafu ukiyeyuka kwa kasi: UNEP

Shirika la mpango wa Mazingira katika Umoja wa Mataifa, UNEP, limeonya kuwa ongezeko la joto duniani huenda likawa juu zaidi ikiwa udongo wenye barafu ulioko kwenye maeneo ya kaskazini mwa dunia utaendelea kuyeyuka kwa kasi ya sasa.

Udongo huo, uitwao Permafrost katika lugha ya Kiingereza, umeenea kwa takriban robo ya eneo lote la kaskazini mwa dunia, na una viwango vya kaboni mara mbili zaidi ya kiwango kilichoko angani sasa.

Katika ripoti yake ambayo imetolewa wakati wa mkutano kuhusu mabadiliko ya hali ya hewa unaoendelea mjini Doha, Qatar, UNEP inaonya kuwa Permafrost ikipata joto na kuyeyuka, huenda ikabadili mifumo ya mazingira na kusababisha hasara kubwa kwa miundo mbinu kwa sababu ya ardhi isiyo thabiti. Utabiri wa mabadiliko ya hali ya hewa haujawahi kuhusisha athari za kuyeyuka Parmafrost.

Miongoni mwa washiriki wa mkutano huo wa Doha ni Dkt. Richard Muyungi, Mwenyekiti wa Kamati ya Sayansi na Taaluma ya Mabadiliko ya mabadiliko ya tabia nchi kidunia na anafafanua zaidi madhara hayo na hatua za kuchukua.