Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

UNHCR yaadhimisha siku 16 za kupinga dhuluma za ngono

UNHCR yaadhimisha siku 16 za kupinga dhuluma za ngono

Kamishna Mkuu wa Shirika la Kuhudumia Wakimbizi katika Umoja wa Mataifa, Antonio Guterres, amerejelea ahadi ya shirika hilo kujitolea kukabiliana na dhuluma za ngono na kijinsia, akisema kwamba UNHCR imeongeza juhudi zake mwaka huu kuwasaidia waathiriwa kupata haki.

Bwana Guterres amesema, ingawa kuna ufahamu mkubwa wa dhuluma za ngono na jinsia na juhudi za kuzipinga, bado idadi kubwa ya wanawake wanakumbana na jinamizi hili la ukiukaji wa haki zao kwa sababu hasa ya ukosefu wa usawa wa kijinsia unaoendelea kuwepo duniani.

Bwana Guterres amesema hayo katika ujumbe wake kuadhimisha siku 16 za kupinga dhuluma za kijinsia, akitaja kwamba ni muhimu kuendelea kufanya kuzuia na kuitikia dhuluma kama hizo kuwa suala la kipaumbele katika ngazi zote za utendaji kazi. Amesema ametenga dola milioni 6.9 kwa ajili ya miradi ya kukabiliana na dhuluma za ngono na kijinsia katika nchi 12.

Amesema Shirika la UNHCR linakabiliana na hali kadhaa za dharura za kuwalinda wakimbizi, na kwamba limekuwa likipokea ripoti za kuhuzunisha za ubakaji mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo, DRC, ambako kumekuwa na mapigano makali tangu kati mwa mwezi Novemba. Jason Nyakundi na taarifa kamili