Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Pillay asikitishwa na hali ya raia walobaniwa kwenye mzozo wa Gaza

Pillay asikitishwa na hali ya raia walobaniwa kwenye mzozo wa Gaza

Kamishna Mkuu wa Haki za Binadamu, Navi Pillay, ameelezea masikitiko yake kuhusu hali ya raia waliobaniwa kwenye mzozo kati ya Israel na Palestina Gaza na kusini mwa Israel.

Bi Pillay ameelezea kushangazwa kwake na kuongezeka kwa idadi ya raia wa Palestina, wakiwemo wanawake na watoto, ambao wameuawa au kujeruhiwa katika kipindi cha masaa 48 yaliyopita kutokana na hatua za kijeshi za Israel.

Kwa mujibu wa habari zilizokusanywa na waangalizi wa ofisi ya haki za binadamu walioko kwenye maeneo hayo, idadi ya raia waliouawa imezidi maradufu katika muda huo wa siku mbili. Kufikia Jumanne asubuhi, yapata raia 57, wakiwemo watoto, wameuawa huku mamia yaw engine wakijeruhiwa tangu Novemba 14.

Kamishna Pillay amesema anaunga mkono kwa dhati juhudi za Katibu Mkuu za kujaribu kufikia mkataba wa kusitisha mapigano, na anataraji kuwa mkataba wowote kama huo utakuwa na azimio la kila upande kuheshimu sheria ya kimataifa ya haki za binadamu na ile ya kibinadamu. Rupert Colville ni msemaji wa ofisi ya Kamishna Mkuu wa Haki za Binadamu

(SAUTI YA RUPERT COLVILLE)