Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Baraza la Usalama laazimia kuongeza muda wa kikosi cha UM Abyei

Baraza la Usalama laazimia kuongeza muda wa kikosi cha UM Abyei

Baraza la Usalama, leo kwa kauli moja limeazimia kuongeza muda wa kikosi cha kulinda amani cha Umoja wa Mataifa katika eneo la Abyei (UNISFA) hadi tarehe 31 Mei 2013. Eneo la Abyei lililoko kwenye mpaka kati ya Sudan na Sudan Kusini, limekuwa likizozaniwa kwa muda na nchi hizo mbili.

Baraza hilo la Usalama pia limezitaka nchi hizo mbili zikamilishe mipango ya kuweka mamlaka za uongozi katika eneo hilo, pamoja na huduma za polisi wa usalama, chini ya mktaba ulosainiwa mwezi Juni mwaka 2011 mjini Addis Ababa, na ambao ulitaka yawekwe mamlaka ya muda katika eneo hilo, pamoja na kuondolewa kwa majeshi ya pande zote mbili.

Miongoni mwa majukumu ya kikosi hicho cha UNISFA, ni kuhakikisha usalama na kusimamia shughuli za kuondoa majeshi ya nchi hizo mbili kutoka eneo hilo la Abyei.

Mkutano huo wa Baraza la Usalama umehudhuriwa pia na wawakilishi wa Sudan na Sudan Kusini, ambao wamelishukuru baraza hilo kwa uamuzi wake.