Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Mikakati rahisi yaweza kutumika kupunguza vifo vya watoto wanaozaliwa njiti: WHO

Mikakati rahisi yaweza kutumika kupunguza vifo vya watoto wanaozaliwa njiti: WHO

Tatizo la watoto kuzaliwa njiti au kabla ujauzito haujatimiza wiki 37 linaongoza kwa kusababisha vifo vya watoto wachanga Milioni Moja duniani kote, wakati ambapo asilimia 75 ya watoto hao wanaweza kuokolewa kwa kutumia teknolojia rahisi na kwa gharama nafuu.

Huo ni ujumbe wa leo ambayo ni siku ya kimataifa ya kupambana na vifo vya watoto wachanga wanaozaliwa njiti, ujumbe ambao unatolewa ili kuhamasisha mataifa kukabiliana na hali hiyo inayosababisha ulemavu na wakati mwingine vifo.

WHO inasema kuwa pamoja na kwamba watoto hao huzaliwa wakiwa hai lakini wanakuwa hatarini zaidi kupata maambukizo ya magonjwa mbali mbali.

Takwimu za WHO zinaonyesha kuwa nchi zenye idadi kubwa ya watoto wanaozaliwa njiti ni India, China, Nigeria, Pakistani, Indonesia, Marekani, Bangladesh, Ufilipino, Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo na Brazil. Elizabeth Mason ni Mkurugenzi katika WHO katika idara ya afya ya uzazi, watoto na vijana.

Mfumo wa kinga ya mwili unakuwa bado haujakomaa iwapo wanazaliwa kabla ya muda na wanahitaji dawa za kuzuia uambukizo kwa watoto wachanga. Malawi inaongeza jitihada za kupunguza vifo kwa kutumia mtindo wa uitwao Kangaroo ambao mama humbeba mtoto wake mchanga kifuani huku akiwa amemfunika kwa ajili ya kumpatia joto . Argentina inawaweka pamoja watoto wote waliozaliwa njiti na sasa wamekuwa watoto wakubwa au watu wazima na inatarajia kuingia kwenye kitabu cha maajabu ya dunia cha Guiness kwa kuwa na idadi kubwa zaidi ya watoto njiti waliowekwa pamoja.”