Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

UM waadhimisha miaka 60 ya huduma yake ya kutoa maelezo kwa wageni kuhusu shughuli zake

UM waadhimisha miaka 60 ya huduma yake ya kutoa maelezo kwa wageni kuhusu shughuli zake

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-Moon amesema maelezo wanayopata wageni kuhusu shughuli za umoja huo pindi wanapotembelea makao makuu yake mjini New York, yamesaidia kutoa picha halisi na kwa wakati muafaka kuhusu chombo hicho na kuepusha taarifa zisizo sahihi.

Bwana Ban amesema hayo wakati wa sherehe za kuadhimisha miaka 60 ya shughuli ya utoaji wa maelezo kwa wageni wanaotembelea ofisi za Umoja wa Mataifa mjini New York, Marekani iliyohudhuriwa na wageni mbali mbali wakiwemo wafanyakazi wanaotoa maelezo kwa sasa na wale wa zamani.

Amesema katika miaka 60, wageni Milioni 40 walitembelea Umoja wa Mataifa na kupatiwa maelezo kutoka kwa watoa maelezo wa ziara hizo wanaotoka kona mbali mbali za dunia ambao hufanya kazi yao kwa weledi na hatimaye wengine kuingia katika ajira zingine ndani ya Umoja huo.

Alice Kariuki wa idhaa hii alifanya kazi hiyo kwa miaka Miwili kuanzia mwaka 1990 na anazungumzia uzoefu wake.