Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Ban ahimiza uchaguzi wa amani Sierra Leone

Ban ahimiza uchaguzi wa amani Sierra Leone

Katika ujumbe mwingine, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki-Moon, ametoa wito kwa raia wa Sierra Leone wahakikishe kuwa moyo wa amani ambao umekuwepo katika harakati za uchaguzi kufikia sasa, utadumishwa hata kwenye siku ya uchaguzi, kuhesabu kura na wakati matokeo yatakapotangazwa.

Taifa la Sierra Leone linajiandaa kufanya uchaguzi wa tatu tangu kumalizika vita vya wenyewe kwa wenyewe, ili kumchagua rais, wabunge na viongozi wa mitaa, mnamo Jumamosi tarehe 17 Novemba.

Katibu Mkuu amevipongeza vyama vya kisiasa vilivyojiandikisha, taasisi za kitaifa na wadau wengine kwa ushirikiano wao kufuatia kutia saini azimio la Mei 18 mwaka 2012, ambapo wote walijitolea kuhakikisha kuna uchaguzi wa amani, ambao ni huru na wa haki. Amesema uchaguzi wa amani na matokeo ya kusadikika ni muhimu katika kuimarisha amani iliyopatikana kwa njia ngumu nchini humo, na kuonyesha kwamba hatua zilizopigwa tangu kumalizika migogoro mwongo mmoja ulopita haziwezi kurudi nyuma.

Ameongeza kuwa Umoja wa Mataifa utaendelea kuunga mkono juhudi za Sierra Leone kujenda taifa lenye amani, demokrasia na maendeleo.