Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Vifaa vya msaada kwa ajili ya raia wa Syria vyaharibiwa katika shambulio

Vifaa vya msaada kwa ajili ya raia wa Syria vyaharibiwa katika shambulio

Nchini Syria matukio mawili ikiwemo shambulio la bomu na utekaji nyara nchini yamesababisha kuharibiwa kwa vifaa vya misaada vilivyokuwa visambazwe kwa raia wa nchi waliokimbia makazi yao kutokana na ghasia.

Shirika la kuhudumia wakimbizi la Umoja wa Mataifa, UNHCR limesema katika tukio la kwanza mablanketi Elfu Kumi na Tatu yaliyokuwa yamehifadhiwa kwenye ghala la shirika la mwezi mwekundu la Syria huko Aleppo yameharibiwa kutokana na shambulio la bomu.

Halikadhalika lori lililokuwa limebeba mablanketi 600 lilitekwa nyara na watu wasiofahamika wakati likiwa njiani kueleka mji wa Adra nje kidogo ya mji mkuu wa Syria, Damascus.

UNHCR inasema operesheni zake huko Damascus zinakwamishwa na hali mbaya ya usalama huku wafanyakazi wake huko Hassakeh, kaskazini mashariki mwa Syria, wakilazimika kuondolewa kwa muda.

Hata hivyo msemaji wa UNHCR Melissa Fleming anasema licha ya kuzorota kwa usalama, wameweza kutoa vifurushi vya misaada kwa familia zenye mahitaji kwa ajili ya msimu wa baridi kali unaokaribia.

(SAUTI YA MELISSA FLEMMING)