Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

UM waomba dola milioni 39 zaidi kuisaidia serikali ya Haiti kukabiliana na athari za kimbunga Sandy

UM waomba dola milioni 39 zaidi kuisaidia serikali ya Haiti kukabiliana na athari za kimbunga Sandy

Naibu Mkuu wa ofisi ya kuratibu misaada ya kibinadamu katika Umoja wa Mataifa, Catherine Bragg, leo amezindua ombi la dola milioni 39, kama marekebisho ya ombi la awali la ufadhili wa misaada ya dharura nchini Haiti, ili kukabiliana na athari za kimbunga Sandy. Fedha hizo zinahitajika ili kukabiliana na matatizo ya uhaba wa chakula, makazi, huduma za afya na maji kwa mamilioni ya watu. Milioni 22 kati ya fedha hizo zinahitajika kwa mahitaji ya dharura zaidi mwaka huu.

Kimbunga Sandy kiliipiga Haiti mnamo tarehe 23 Oktoba, na kuwaua watu 54, huku kikiwaacha maelfu ya wengine bila makazi, bila huduma muhimu baada ya siku tatu mfululizo za mvua. Watu milioni moja na nusu sasa hawana usalama wa chakula, huku asilimia 2 ya watoto chini ya miaka mitano, ambao tayari walikuwa hawana chakula, sasa wana matatizo ya utapia mlo ulokithiri.

Serikali ya Haiti imetangaza mwezi mmoja wa hali ya dharura katika taifa hilo. Kwa mujibu wa takwimu za serikali, sekta ya kilimo nchini humo imepoteza thuluthi tatu za mazao ya kilimo kwa sababu ya kimbunga Sandy na kile cha Isaac cha Mwezi Agosti, pamoja na ukame.