Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Nishati ya nyuklia bado ni muhimu kukidhi mahitaji ya nchi: India

Nishati ya nyuklia bado ni muhimu kukidhi mahitaji ya nchi: India

Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa leo limeelezwa kuwa nishati ya nyuklia bado ni mbadala muhimu wa kukidhi mahitaji ya nishati duniani licha ya ajali iliyokumba mtambo wa nyuklia wa Fukushima Daiichi nchini Japan mwaka jana.

Afisa wa India kwenye Ubalozi wa nchi hiyo katika Umoja wa Mataifa Annu Tandon ametoa kauli hiyo wakati baraza hilo lilipokuwa linajadili ripoti ya shirika la kimataifa la nishati ya atomiki, IAEA.

Bi. Tandon amesema makadirio ya IAEA ya uwezo wa dunia wa kuzalisha nishati ya nyuklia mwaka 2030 yamekuwa chini kuliko ilivyotarajiwa awali kwa sababu baadhi ya nchi zimefuta maamuzi yao ya kuanzisha miradi ya nyuklia.

Hata hivyo ametaja baadhi ya mambo ambayo yanafanya nchi kuona nyuklia kuwa mbadala wa kukidhi mahitaji ya nishati.

"Ongezeko la mahitaji ya nishati duniani, pamoja na wasiwasi kuhusu mabadiliko ya tabia nchi, ongezeko la mara kwa mara la bei ya mafuta na uhakika wa kupatikana kwa nishati bado vimebaki ni vigezo muhimu vya kuamua kuwa na mchanganyiko wa vyanzo vya nishati. Hii inaonyeshwa bayana katika ripoti hiyo ya ufuatiliaji ambapo licha ya ajali ya nyuklia nchini Japan mwaka 2011, nishati ya nyuklia bado imeonekana ni mbadala muhimu siyo tu kwa nchi zenye miradi ya nyuklia hivi sasa bali pia kwa nchi zinazoendelea ambazo zina mahitaji makubwa ya nishati.”

Halikadhalika Bi. Tandon amesema nishati ya nyuklia bado ina nafasi kubwa katika ukuaji wa uchumi endelevu nchini India.