Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Zaidi ya watu Bilioni 2.2 wako hatarini kukumbwa na Malaria huko Asia–Pasifiki

Zaidi ya watu Bilioni 2.2 wako hatarini kukumbwa na Malaria huko Asia–Pasifiki

Zaidi ya watu Bilioni 2.2 katika nchi za Asia-Pasifiki wako hatarini kukumbwa na ugonjwa wa Malaria, ugonjwa ambao kwa kiasi kikubwa umekuwa ukitajwa kuwa tishio barani Afrika pekee.

Taarifa hizo ni kwa mujibu wa ripoti mpya ya mpango wa ushirikiano wa kimataifa wa kudhibiti Malaria, RBM ambayo imesema nchi za India, Myanmar, Papua New Guinea na Indonesia ndio ziko hatarini zaidi katika Ukanda huo.

Ripoti hiyo imetoa mfano kuwa mwaka 2010 eneo hilo lilikuwa na wagonjwa wapatao Milioni 30 wa Malaria ambao kati yao 42,000 walifariki dunia.

Mkurugenzi Mtendaji wa ushirikiano huo wa kimataifa wa kudhibiti Malaria , Dkt. Fatoumata Nafo-Traore amesema kuna changamoto kubwa ya kupambana na kutokomeza Malaria kwenye ukanda huo wa Asia-Pasifiki kwa sababu vimelea vya Malaria vimekuwa sugu Artemisinin ambayo ni dawa inayotumika kutibu Malaria.

Ili kuweza kuondokana na dawa hii ambayo vimelea vimekuwa sugu, tunahitaji kutengeneza dawa mpya. Tunahitaji kujenga ushahidi wa udhibiti wa Malaria. Tunahitaji chanjo ambayo itasaidia vita dhidi ya Malaria. Ushiriki wa sekta tofauti katika vita dhidi ya Malaria ni muhimu kwa kuwa Malaria siyo suala la kiafya pekee. Ni suala la maendeleo. Kuwekeza katika hatua za kupambana na Malaria kutapunguza utoro kazini, shuleni na pia itasaidia nyongeza ya vitegauchumi katika maeneo ambayo yameachwa kutokana na tatizo la Malaria.”